Jumamosi, 31 Agosti 2013

Wengi tunafuga nyuki, tunakula asali lakini hatujui kama nyuki wana faida zaidi ya hizi hapa.
Wanasayansi kutoka chuo kikuu cha tiba Washington, Marekani  wamegundua katika utafiti wao kuwa sumu iliyopo katika mwili wa nyuki iitwayo toxin melittin inaweza kuvivunjavunja na kuviharibu virusi vya Ukimwi pasipo kuacha madhara katika chembehai za mwili.
Habari hii imeelezwa katika taarifa ya tiba za dawa za kupunguza makali ya virusi vya Ukimwi iliyotolewa mapema mwaka huu.
Watafiti hawa wanaeleza kuwa matokeo ya utafiti huu kufika katika hatua kubwa inayoleta matumaini ya kupamba na VVU  kwa kuweza kupata dawa ya kupaka ya majimaji ndani ya uke itakayotumika kupambana na maambukizi ya VVU.
Dk Joshua Hood anasema: “Matumaini yetu ni kwa maeneo ambayo hali ya maambukizi yapo juu na vigumu kuzuilika, dawa ya majimaji mazito inaweza kutumika kupaka ndani ya uke katika kuzuia maambukizi ya mwanzoni kabisa.”
Sumu ya nyuki, melittin, imeonyesha uwezo wa kupambana na VVU kwa kuvunja ganda linalomzunguka kirusi na virusi wengine kwa kulitoboa na kuacha matundu.
Mwandishi mwandamizi wa makala za biokemia,  Dk Samuel Wicline, Profesa wa Biochemia wa Taasisi ya Russel Hornsby anafafanua kuwa kuwa vijipande vidogo vilivyoshindiliwa vya sumu ya nyuki vimeonyesha kuwa na tabia ya kuweza kuua chembe hai zenye saratani.
Anaeleza mtaalamu huyo kuwa hii si mara ya kwanza katika ugunduzi wa tiba ya namna hii, kwani mwaka 2004 wanasayansi wa Croatia walitoa taarifa yao katika jarida la sayansi ya chakula na kilimo kuwa mazao ya nyuki, ikiwamo asali na sumu ya nyuki  vina uwezo wa kutumika kutibu na kuzuia saratani.
Chembehai za mwilini zenye afya huendelea kubaki salama pasipo kupata madhara wakati wa tiba kwani sumu hiyo ya nyuki imetengenezewa na kitu kama ngao ambayo ikikutana na seli za mwili hudunda na kwenda mbali bila kujishikiza.
Hii ni kwa sababu ya seli za mwili ni kubwa kimaumbille kuliko sumu ya melittin, wakati kwa  virusi vya Ukimwi ni vidogo kuliko melittin, hivyo ikikutana navyo ngao hiyo haiwezi kuzuia kirusi kidunde kwani ni kidogo, hivyo  kirusi hudakwa na melittin na kushikamana, hivyo kirusi huweza kuharibiwa.
Dk Hood anaeleza kuwa vijipande vilivyoshibishwa na sumu ya melittin huweza kushikamana na kirusi na kutoboa tundu katika ganda la kirusi na kuchana ganda lote, hivyo kirusi huweza kuvunjwa.
Wakati tiba kwa kutumia dawa za kufubaza makali ya VVU, yaani ARVs zinafanya kazi kwa kuzuia uwezo wa virusi kujidurufisha, kwa tiba ya melittin hushambulia sehemu muhimu ya kimaumbile ya  virusi ambayo ndiyo nguzo imara kwa virusi

Ijumaa, 30 Agosti 2013

 Tume ya Vyuo vikuu nchini (TCU) imetoa majina ya wanafunzi waliodahiriwa kwa mwaka wa masomo wa 2013/2014 ambao wameonekana kuchaguliwa kwa chuo zaidi ya kimoja.Zaidi tembelea tovuti kwa kubofya hapa chini
                 < http;/www.tcu.go.tz >


MAZITO tena yameibuka kuhusu yule trafiki feki James Hussein, mkazi wa Kimara Matangini, jijini Dar es Salaam ambaye yuko Gereza la Segerea, Dar akikabiliwa na kesi ya kujifanya askari wa usalama barabarani.

Habari za ndani kutoka Gereza la Isanga, Dodoma zinadai kuwa, trafiki huyo ana mambo mengi ya kushangaza ambayo Watanzania wengi hawayajui.

Askari traffic  feki mwenye majina mengimengi tofauti

Mtoa habari wetu alisema kuwa, James Hussein si jina halisi la trafiki feki huyo. Alisema jina lake halisi ni Ali Kinanda.

“Yule jamaa anaitwa Ali Kinanda, sisi kumwona kwenye picha gazetini akijiita James Hussein tulishangaa sana,” kilisema chanzo chetu.

Chanzo kikazidi kudai kwamba, kuanzia mwaka 1984 jamaa huyo alikuwa ni askari magereza katika Gereza la Butimba, Mwanza hadi mwaka 1987 alipoacha.

Mtoa habari wetu aliendelea kumwanika trafiki feki huyo kuwa, mwaka 2002 mtuhumiwa huyo alidaiwa kupata msala wa tukio la ujambazi lililotokea Mpwapwa, Dodoma ambapo kesi yake iliunguruma hadi mwaka 2003 ambapo hukumu ilitolewa yeye na wenzake kwenda jela miaka 30.

“Mwaka 2002 mpaka 2003, Kinanda alipata kesi ya ujambazi akiwa na wenzake, sikumbuki idadi yao. Kesi iliisha kwa hukumu ya miaka 30 jela kwenye Gereza la Isanga hapa Dodoma,” alisema mnyetishaji huyo.

“Akiwa gerezani, Kinanda alionekana mtiifu kiasi kwamba alipewa cheo cha kusimamia wenzake, yaani mnyapara wakiamini anaendelea vizuri na kifungo chake hicho.

“Hakuna aliyejua kama jamaa anaweza kutoroka. Ama kweli moyo wa mtu anaujua mwenyewe. Hivi hapa (Gereza la Isanga) wafungwa wenzake wameshangaa kusikia jamaa amekuwa trafiki huko Dar es Salaam,” kilidai chanzo.

Habari zaidi ziliendelea kudai kwamba, Desemba 10, 2012 akiwa gerezani, mfungwa huyo alitoroka katika mazingira ya kutatanisha akiwa chini ya uangalizi wa askari magereza aliyejulikana kwa jina moja la Shaibu.

Ilidaiwa kuwa, baada ya picha yake kuonekana kwenye gazeti, askari magereza wa Isanga waliutaarifu uongozi mara moja ambapo nao ulituma wachunguzi jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuanza mchakato wa kumtia mikononi mfungwa huyo ili akamalizie kifungo chake cha miaka thelathini jela.

Inadaiwa kuwa, wachunguzi hao ambao ni askari magereza wapo Dar wakisubiri siku ya kesi ya kujifanya trafiki itakapopelekwa kusikilizwa kwa hakimu.

Wakati mnyetishaji wetu kutoka gerezani Isanga Dodoma akianika madai ya siri hiyo nzito, Agosti 26, mwaka huu jijini Dar es Salaam, Mwandishi Wetu, alipata taarifa kuwa, mtuhumiwa huyo wa kutenda kosa la kujifanya trafiki amefariki dunia ghafla akiwa gerezani Segerea.

Ilibidi mwandishi wetu amtafute Msemaji wa Jeshi la Magereza Tanzania, Meja Mtiga Omar na kumuuliza kuhusu madai hayo ya kifo ambapo alisema:

“Si kweli kwamba amekufa, bali ana tuhuma nyingine ya kutoroka gerezani ambapo tutamfungulia mashitaka mengine ya kutoroka akiwa gerezani anatumikia kifungo chake.”

Juhudi za kumpata Mkuu wa Gereza la Isanga, Dodoma zilishindikana baada ya simu yake ya mkononi kuita kwa muda mrefu bila kupokelewa.

James Hussein kama ndiye Ali Kinanda yupo Gereza la Segerea, hadi Septemba 5, 2013 kesi yake itakaporudi tena mbele ya Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Ilala, Joyce Minde kwa ajili ya kusikilizwa.