Alhamisi, 26 Septemba 2013




MKAGUZI na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), amebaini madudu katika matumizi na mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya.

Kutokana na upungufu huo, CAG amewataka madiwani kuchukua hatua ili waliosababisha ufujaji huo wa fedha wachukuliwe hatua za kisheria.

Upungufu huo upo katika baadhi ya miradi ya maendeleo chini ya mfuko wa LGCDG yenye thamani ya sh 326,208,530 ambayo haikukamilika na fedha hazionekani.

Mradi mwingine ni ule ulio chini ya mfuko wa MMAM, wenye thamani ya sh 218, 349, 260 ambao nao haukukamilika na fedha hazionekani.

CAG aliitaja miradi mingine kuwa ni madawa yenye thamani ya sh 9,867,005 yaliyoharibika, lakini hayakufutwa na kuondolewa kwenye vitabu, mradi wa thamani ya sh 208,140,250 wa mfuko wa ASDP uliokamilika, lakini hautumiki kana kwamba fedha zilizotumika ziliokotwa, pamoja na mradi wa barabara yenye thamani ya sh 181,146,200 ambao haujakamilika na fedha zilizotengwa hazionekani.

Pamoja na upungufu huo wa msingi, mkaguzi katika taarifa yake alibaini hoja zilizojadiliwa na kufungwa katika mwaka 2011/2012 ni 37 kati ya 79 wakati 42 hazijafungwa. Zitakaguliwa na kujadiliwa tena mwaka 2012/2013.

Aidha, katika kikao cha Kamati ya Fedha, Uongozi na Mipango cha kupitia hoja za CAG kilichofanyika katika ukumbi wa Community Center Julai 22, 2013 na Baraza la Madiwani lililofanyika Septemba 4, 2013, baada ya kubainika kuwepo na upungufu kadhaa wakuu wa idara na madiwani walipewa ushauri kuufanyia kazi.

Mwenyekiti wa kikao hicho ambaye pia ni Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Abbas Kandoro alitoa ushauri kwa watendaji na wataalamu ambao aliwataka wazingatie kanuni, taratibu, miongozo na sheria za fedha na manunuzi ya umma, na pia aliwataka wataalamu hao kutoa ushirikiano kwa wakaguzi wa ndani na nje pindi wanapokuja kukagua ili kuleta ufanisi katika kutekeleza shughuli zao.

Aliendelea kuwataka wataalamu kusimamia matumizi ya sheria ndogo ndogo za kuzuia magonjwa ya mifugo ambayo inawataka wafugaji kutumia kikamilifu majosho kwa kuogesha mifugo yao, na kuwa aliwataka wataalamu kuandaa sera na mpango kwa ajili ya kuzuia majanga na hasara kwa wahanga (Risk and Fraund Assessment Policy) ikiwamo mpango wa kuhakikisha dawa, vifaa tiba, vitendanishi na vifaa chakavu vilivyokwisha muda wa matumizi vinateketezwa.

Mkuu huyo wa mkoa aliwataka madiwani na watendaji kushirikiana katika kufanya shughuli za wananchi kupitia halmashauri ya wilaya kwa kuwa tayari imepata hati ya shaka kutokana na utendaji mbaya na kwamba wasipokuwa makini kuna uwezekano wa kupata hati chafu.

Wananchi kwa upande wao waliokuwepo katika kikao hicho kilichokaliwa siku za hivi karibuni walishangazwa na taarifa hizo za ubadhirifu uliofanywa katika halmashauri hiyo na kupata wasiwasi juu ya uwezo duni wa madiwani wao ambao mbali na kupewa ushauri na mkuu wa mkoa wameshindwa kuchukua hatua kwa watendaji waliokwamisha shughuli za maendeleo.
Imeandaliwa na Ibrahim Yassin (Kyela)

Jumatano, 25 Septemba 2013




Zaidi ya wanafunzi 300 wa elimu ya juu wa vyuo mbalimbali watakosa mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kutokana na kushindwa kujaza fomu za kuomba mikopo katika kipindi kilichowekwa.
Watakaokosa mikopo hiyo kwa mwaka wa masomo wa 2013/2014 ni kuanzia mwaka wa pili na kuendelea, ambao hawakujaza fomu za kuonyesha taarifa zao mpya kwa bodi.
Wanafunzi hao walitakiwa kuwasilisha maombi ya kupewa mikopo kati ya Mei hadi Julai 30, mwaka huu.
Mkugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HELSB, Cosmas Mwaisobwa, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi kuhusu utendaji wa kazi wa bodi hiyo.
Mwaisobwa alisema kwa kuwa wanafunzi hao hawakujaza fomu za kuomba mikopo, mwaka huu hawatapata fursa hiyo na kwamba kwa mujibu wa utaratibu wao, kila mwaka lazima mwanafunzi aombe.

Alisema wanafunzi watakaokosa fursa hiyo ya mikopo wameanza masomo yao katika vyuo mbalimbali nchini na kwamba  HESLB haijui sababu zilizowafanya wasiombe.
Kuhusu ufanisi katika utoaji wa mikopo, Mwaisobwa alisema idadi ya wanafunzi wanaoomba mikopo imeongezeka kutoka 42,729 mwaka 2005/2006 hadi kufikia wanafunzi 97,348 mwaka 2012/2013.
Aidha, Mwaisobwa alisema bajeti ya kuwakopesha wanafunzi imeongezeka kutoka Sh. bilioni 56.1 mwaka 2005/2006 hadi kufikia Sh. bilioni 306 mwaka 20012/2013.
Alisema mwaka huu serikali imeitengea bodi hiyo Sh. bilioni 325 kwa ajili ya kuwakopesha wanafunzi wapya, 31,647 na 62,376 wanaondelea na masomo yao katika vyuo mbalimbali.
Wakati wanafunzi hao wakikosa fursa ya mikopo, mapema mwezi huu, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, aliitaka bodi hiyo kuendelea kutoa huduma kwa ufanisi na weledi mkubwa kwa mwaka huu wa masomo ili kuepusha migogoro ya wanafunzi kuhusu mikopo.

Kaimu Katibu Tawala mkoa wa Mbeya Leonard Magacha akisaini katika kitabu cha wageni baada ya kuwasili katika viwanja vya TIA kushiriki mashindano ya ngoma za asili. 

WANANCHI wameaswa kupenda utamaduni wa Asili hususani ngoma za Makabila ili kuenzi mila na desturi zilizoachwa na mababu  tangu zamani na siyo kuegemea katika nyimbo za kizazi kipya.
Mwito huo ume na Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya, Leonard Magacha wakati akifungua mashindano ya Ngoma za Asili yaliyofanyika katika Viwanja vya Chuo cha Uhasibu(TIA) Jijini hapa.
Magacha amesema mashindano ya ngoma za asili yatasaidia kuamsha ari ya kupenda utamaduni wa Mtanzania kwa kuenzi Mila na Desturi zilizoachwa na waliotanguliatangu zamani kabla ya sayansi na teknolojia ambapo vifaa vya asili vilitumika.
Ameongeza kuwa kupitia mashindano hayo itakuwa chachu ya kufufua utamaduni vijijini ikiwa ni pamoja na kupima utendaji kazi wa Maafisa utamaduni wa Wilaya kwa kuhamasisha na kuwafundisha wananchi kuzipenda ngoma za asili.
Kwa upande wake Afisa Michezo na Utamaduni wa Mkoa wa Mbeya, George Mbigima, amesema kama Mkoa utandaa mashindano makubwa mwakani ambayo yataanzia kwenye ngazi ya Kijiji, kata, Wilaya na hatimaye kumpata mshindi wa Mkoa.
Naye Mkuu wa Matukio wa kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kanda ya Mbeya, Geophrey Mwangungulu ambao ndiyo waandaaji wa Mashindano hayo amesema lengo la kuandaa tukio hilo ni kuhamasisha wananchi kupenda ngoma za asili pamoja na utamaduni.
Amesema jumla ya vikundi 26 vilijitokeza kushiriki mashindano hayo kutoka katika Wilaya za Mbeya, Rungwe, Kyela,Mbozi Njombe na Iringa ambapo katika Mashindano hayo Mshindi wa Kwanza aliibuka na kitita cha fedha taslimu Milion moja na Kikombe.
Mshindi wa pili aliibuka na shilingi laki tano huku mshindi wa Tatu akiondoka na shilingi laki mbili na washiriki wengine wakiambulia kifuta jasho cha shilingi 50,000/= kwa kila kundi.
Katika mashindano hayo yaliyokuwa kivutio kwa mamia ya Wakazi wa Mbeya kikundi cha ngoma cha Kasanga maarufu kwa Ing’oma kutoka Wilayani Rungwe ndiyo walioibuka kidedea katika kinyang’anyiro hicho.
Nafasi ya pili ilienda kwa kikundi cha ngoma za asili cha Lipango kutoka Isansa Wilayani Mbozi na Nafasi ya Tatu ikinyakuliwa na Kikundi cha Mbeta kutoka Isyesye Jijini Mbeya.

Mkuu wa matukio Geophrey Mwangunguru akizungumza na wananchi waliofurika kushuhudia mashindano hayo.
Mgeni rasmi Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya akizungumza na mamia ya Wananchi na washiriki wa Mashindano ya ngoma za asili. 
Baadhi ya Watumishi wa TBL pamoja na viongozi mbali mbali wakifuatilia kwa makini burudani zilizokuwa zikiendelea kutoka kwa washiriki.
Majaji wakifuatilia kwa makini Washiriki kama wanafuata vigezo na masharti ya mashindano na kuchukua alama.
Mkuu wa matukio akiwa ameshika kikombe atakachojishindia mshindi wa kwanza katika kucheza na kuimba ngoma za asili.
Mmoja wa Majaji Nimwindael Mjema akisoma washindi wa shindano la ngoma za asili kuanzia nafasi ya 20 hadi ya 4 ambao waliambulia kifuta jasho cha shilingi 50000 kila kundi.

Baadhi ya vikundi vya ngoma za asili wakiwa wamekaa wakipewa maelekezo mbali mbali kabla ya kuanza kwa mashindano
Vikundi vikiwajibika uwanjani.
Wananchi mbali mbali wakifuatilia mashindano hayo
Mzee wa mila ambaye pia ni kiongozi wa kikundi cha ngoma cha Kasanga kutoka Tukuyu Wilayani Rungwe akiwa ameshikilia kombe na fedha taslimu shilingi Milion Moja baada ya kuibuka washindi wa kwanza wakicheza ngoma yao aina ya Ling'oma.