
Jumanne, Agosti 20, 2013

Unknown
 
 
AFISA
 wa cheo cha juu katika Jeshi la Wananchi (JWTZ), anayeaminika kuwa na 
asili ya Rwanda, ametoweka katika mazingira ya kutatanisha, huku akiacha
 wingu la mashaka kwamba, hatua yake hiyo inaweza ikawa imeambatana na 
kupotea pia kwa baadhi ya taarifa muhimu za kijeshi.
Taarifa
 za kutoweka kwa ofisa huyo mwenye cheo cha luteni kanali, zinalihusisha
 tukio hilo na hatua za makachero wa JWTZ kufuatilia nyendo zake na 
zililifikia gazeti la MTANZANIA Jumapili kwa mara ya kwanza katikati ya 
wiki hii.
Vyanzo vya habari vya kuaminika vinaeleza 
kuwa, tayari maofisa wa JWTZ wameshaanza kufuatilia kwa karibu tukio la 
kutoweka kwa ofisa huyo, ambalo pia limezusha hali ya sintofahamu 
kwamba, huenda akawa ameondoka na nyaraka nyeti za kijeshi.
Kabla
 ya kutoweka ofisa huyo, ambaye nyendo zake zimekuwa katika darubini 
kali za makachero wa JWTZ, alikuwa akifanya kazi katika kitengo cha 
teknolojia ya mawasiliano ya kijeshi (IT).
Hatua ya 
kutoweka kwa ofisa huyo wa juu wa JWTZ anayetajwa kwa jina moja la 
Selumbo, imekuja siku chache tu baada ya kuibuka kwa msuguano wa kauli 
baina ya Ikulu ya Dar es Salaam na ile ya Kigali. 
Chanzo
 cha msigano huo wa maneno uliogeuka na kuwa mzozo wa kidiplomasia, ni 
ushauri uliotolewa na Rais Jakaya Kikwete kwa Rais Paul Kagame wa 
kumtaka awe tayari kukaa meza moja na waasi wa kundi la FDLR wanaopigana
 Rwanda, kutoka mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC). 
Tayari
 msigano huo wa Kikwete na Kagame umeanza kutajwa na baadhi ya wadadisi 
wa mambo kuwa tishio kubwa la kwanza la ustawi, uimara na misingi ya 
mshikamano ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambayo mataifa hayo 
mawili ni wanachama wake.
Siku chache baada ya 
ushauri huo, Kagame alinukuliwa na vyombo mbalimbali vya habari nchini 
Rwanda akimkejeli Kikwete, hata kufikia hatua ya kutoa kauli zenye 
mwelekeo wa vitisho dhidi yake.
Kauli hizo za Kagame
 zilisababisha Rais Kikwete, kupitia katika hotuba yake ya mwishoni mwa 
Julai, kujibu mashambulizi, huku akieleza bayana kushangazwa na 
kushtushwa na kejeli na matusi yaliyokuwa yakielekezwa kwake.
Akitumia
 maneno ya kidiplomasia ambayo yametafsiriwa na baadhi wa wachambuzi wa 
masuala ya diplomasia na sayansi ya siasa kuwa yanabeba ujumbe mzito, 
Rais Kikwete alisema alikuwa amesikia yote yanayosemwa kutoka Rwanda na 
alikuwa hakusudii kuyapuuza.
Kauli hiyo ya Kikwete 
ambayo ilitanguliwa na ile aliyoitoa siku chache mkoani Kagera ya 
kuwataka wahamiaji haramu kuondoka nchini, ilifuatiwa na matukio ya 
kuondoka nchini kwa Wanyarwanda wanaokadiriwa kuzidi 5,000.
Wakati
 hali ikiendelea kuwa ni ya mashaka na kutoaminiana kati ya Tanzania na 
Rwanda, katikati ya wiki hii, gazeti dada la MTANZANIA Jumatano, 
lilikuwa na habari kubwa yenye kichwa cha habari kisemacho; ‘Nini 
kinamtia Jeuri Kagame?’ ambayo pamoja na mambo mengine, ilieleza namna 
watu wenye asili ya Rwanda walivyojipenyeza katika taasisi mbalimbali 
nyeti za umma.
Kuvuja kwa taarifa za kurejea Rwanda 
kwa maelfu ya wahamiaji haramu sambamba na hizi za sasa za kutoweka kwa 
ofisa wa juu wa JWTZ kunathibitisha kuhusu kuwapo kwa mwelekeo huo wa 
mambo.
Vyanzo vya habari vya gazeti hili, vinamtaja 
ofisa huyo kuwa ni mmoja wa makachero wenye asili ya Rwanda waliokuwa 
wakifanya kazi ndani ya JWTZ na ambao wanahofiwa kuwa watu wenye 
mawasiliano ya karibu na serikali ya Rwanda, kwa malengo ambayo bado 
hayajawekwa bayana. 
“Ni kweli, huyo ofisa ametoweka
 jeshini na sijui sababu zilizo nyuma yake…hili suala la kuwa anakusanya
 taarifa za siri za jeshi letu na kuzipeleka Rwanda nadhani 
ziligunduliwa na watu wetu ambao wapo kwenye mfumo wa kijeshi,” 
alidokeza mmoja wa watoa taarifa wa MTANZANIA Jumapili.
Msemaji
 wa JWTZ, Meja Erick Komba, alipoulizwa na gazeti hili kupitia simu yake
 ya kiganjani kuhusu ukweli wa taarifa hizo, alishindwa kukubali au 
kukataa, kwa kile alichoeleza kuwa suala hilo ni zito hivyo alikuwa 
akipaswa kuzungumza kwanza na viongozi wake kabla ya kulitolea taarifa.
Meja Komba alieleza kuwa, wanajeshi wanaotoroka ni wengi na wapo waliofungwa kwa kosa hilo la utoro.
“Jamani
 suala hili ni zito, naliogopa, nyinyi hamlioni kama ni zito? Sio kwamba
 sipendi wananchi wapate habari, suala hili tupeni muda kwanza 
tulifanyie ‘analysis’, mbona wanajeshi wengi wanatoroka na hamripoti! 
Waliotoroka ni wengi, wangine wametorokea Rwanda na kwingine na 
wamefungwa. 
“Ni lazima kwanza niongee na mabosi wangu ndiyo nizungumzie vizuri hili… njoo ofisini Jumatatu (Kesho),” alisema Meja Komba. 
Sanjari
 na tukio hilo, taarifa zaidi zilizonaswa na gazeti hili zimedai kuwa 
sasa imebainika pasipo shaka kuhusu kuwapo kwa makachero wa Serikali ya 
Kigali wanaodaiwa kupandikizwa katika taasisi na idara nyeti za serikali
 kwa ajili ya kufanya ushushu kwa maslahi ya Rwanda.
Inadaiwa
 kuwa intelijensia ya JWTZ iliyo na mizizi ndani na nje ya nchi ilibaini
 mapema kuwapo kwa majasusi wa Kinyarwanda ndani ya mfumo wa dola na 
nyendo zao zimekuwa zikichunguzwa kwa muda mrefu na zilibainisha hali 
hiyo.
- Source: Mtanzania
 
 
 
 
 
 
                              
                          
 
  
 
 
 
 
 
 
0 comments :
Chapisha Maoni