Sheikh Mkuu wa Wilaya ya Kyela , Nuhu Mwafilango 
ameelezea jinsi alivyopigwa nondo alipokuwa akiendesha ibada na kudai 
kuwa zilikuwa njama za muda mrefu za kundi la Waislamu wanaharakati 
wanaoipinga Bakwata na aliyempiga alikuwa mwanafunzi wa kidato cha tatu.
                
              
Katika Ibada ya Sikukuu ya Idd, saa 2.15 asubuhi 
iliingia dosari baada ya kuzuka vurugu kubwa katikati ya ibada hiyo 
kutokana na muumini mmoja kuinuka ghafla kwenye msikiti mkuu wa Wilaya 
ya Kyela na kumshambulia Sheikh huyo na watu wengine watatu kujeruhiwa.
                
              
Akizungumzia tukio hilo Sheikh Mwafilango mwenye 
umri wa miaka (76) alisema kuwa vurugu hizo zilitokea katikati ya ibada 
alipokuwa akiongoza swala na baada ya kumaliza takbira saba.
                
              
“Baada ya kuanza kusujudu kwenye ardhi ndipo 
ghafla nikaanza kupigwa na fimbo mgongoni na ndipo nilipotoa kauli ya 
kuwaeleza waumini wenzangu kuwa nimevamiwa na nilipopata nafasi ya 
kuinuka nikapigwa na kitu kama nondo eneo la goti kwenye mguu wa kushoto
 na mkononi,” alisema.
                
              
Alisema kuwa hali ilikuwa ni mbaya katika msikiti huo kwani vurugu zilikuwa kubwa.
                
              
“Kumbe yule kijana aliyenipiga mimi hakuwa peke 
yake bali alikuwa na kundi la watu wengi ambao walikuwa wameshika silaha
 mbalimbali ikiwa ni pamoja na mkasi, kisu na nondo,” alisema.
                
              
Aidha sheikh huyo alisema mbali ya tukio hilo pia 
Agosti 2, mwaka huu alivamiwa katikati ya ibada ya Ijumaa na mmoja wa 
watu waliohusika katika tukio hilo na kumnyang’anya kipaza sauti na 
kumtaka aache kuongoza ibada hiyo.
                
              
“Aliyenivamia siku ya ibada ya Ijumaa alikuwapo 
kwenye tukio hilo la juzi na siku hiyo alichokifanya alitaka mimi 
niondoke na akamwita kijana mdogo kuwa ndiye aendelee kuongoza ibada 
hiyo kitu ambacho waumini waliokuwapo walizuia na kuniruhusu kuendelea 
kuongoza ibada,” alisema.
                
              
Alisema baada ya kuvamiwa alitoa taarifa kwa Mkuu 
wa Wilaya ya Kyela na baadaye kwa mkuu wa polisi wa wilaya ambapo alitoa
 taarifa ya maandishi ya kwamba alivamiwa alipokuwa akiswalisha.
Jumatano, Agosti 14, 2013
Unknown
0 comments :
Chapisha Maoni